MADIWANI mkoani Katavi, wametakiwa kuwa mabalozi wa kwanza kuhamasisha kilimo cha zao la pamba kwa vitendo mkoani humo, ili kuleta hamasa kwa wananchi kulima zao hilo na hivyo kuondokana na umasikini.
Rai hiyo imetolewa na Balozi wa zao la Pamba nchini, Aggrey Mwanri ukumbi wa mikutano wa Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika katika kikao cha tathmini ya kampeni kuhamasisha wananchi kushiriki kilimo cha zao la pamba.
Mwanri amewaambia madiwani kuwa endapo kila diwani ataamua kulima ekari moja ya pamba katika eneo lake, kwa kuzingatia kanuni na mbinu za kisasa, itatoa hamasa kubwa kwa wananchi kushiriki kilimo cha pamba jambo litakaloleta mapinduzi makubwa ya kiuchumi Wilaya ya Tanganyika na Mkoa wa Katavi.
Amesema ni muhimu uongozi kuhamasisha wananchi kuzalisha mazao mbalimbali kwa ziada, ili kukuza uchumi na kuleta maendeleo.