SHEHE wa Mkoa wa Dar es Salaam, Walid Omar amesema watazifungia madrasa zote ambazo zitaonekana zikivunja maadili ya dini ya Kiislamu bila ya kujali inamilikiwa na nani.
Akizungumza na mwandishi wa HabariLEO ofisini Magomeni mkoani Dar es Salaam, alisema wamekuwa wakifanya uchunguzi kila siku kupitia Waislamu wenyewe pamoja na taasisi zingine.
Alisema ikibainika kwamba kuna madrasa inajihusisha na uvunjifu wa maadili wataifunga kwa kuwa kazi ya Waislamu ni kulinda maadili siku zote.
“Nikiwa kama kiongozi wa dini ya Kiislamu kazi yangu saa 24 katika maisha yangu ni kuhakikisha nakemea mmomonyoko wa maadili.
Nasimamia tabia njema, utamaduni na mila zinazokubalika katika jamii,” alisema.
Alitoa wito kwa viongozi wengine wa dini kutoka maeneo mbalimbali, kuhakikisha kwamba wanasimama pamoja kukemea mambo mabaya.