Mafuriko yaathiri kaya 179 Kilombero

MOROGORO; KAYA 179 zinazoishi Kijiji cha Taweta , Kata ya  Masagati , wilaya ya Kilombero , mkoani Morogoro zimekosa mahala pa kuishi  kutokana na nyumba zao kuingiliwa na maji  na  nyingine kubomoka  kufuatia mvua za mafuriko zilizonesha kuanzia juzi.

Diwani wa Kata ya Masagati, Blasius Makao amesema hayo leo Aprili 3,2024 kwa njia ya simu kuwa  mvua hizo zilianza Aprili Mosi mwaka huu  na zimenyesha kwa  siku mbili mfululizo.

Amesema nyumba 15  zimepata madhara makubwa na kati ya hizo saba zimebomoka  na ziliosalia hazina uwezo wa kuhimili kubakia salama, kwani zimeathiriwa vibaya .

Advertisement

Amesema kulingana na kaya hizo, watu wake 895 hawana uwezo kwenda kuishi katika nyumba zao kutokana na kuingiliwa na kiwango kikubwa cha maji.

“Kwa sasa Kata ya Masagati imezingirwa na maji ya mvua za mafuriko kutoka Aprili 1 mwaka huu hadi ninavyoongea leo ( Aprili 3, 2024…watu wanaishi uhamishoni kwenye ofisi ya serikali ya kijiji, ofisi ya kata  na kwenye shule, “ amesema Makao.

Amewaomba wadau mbalimbali kujitokeza kusaidia waathirika hao kwa chakula , mavazi na mahitaji mengine ya kibinadamu katika kipindi hiki kigumu kwao.

Viongozi wa serikali ya mkoa pamoja na Wilaya ya Kilombero wameelekea katika Kata ya Masagati kwa kutumia  usafiri wa anga, ili kujionea hali halisi na namna ya kuchukua hatua mbalimbali za kuwapatia msaada waathirika wa mafuriko hayo.