WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa ameagiza wizara tano zenye dhamana ya kukuza lugha ya Kiswahili kuweka mikakati kuikuza lugha hiyo na kuongeza fursa za kiuchumi kwa Watanzania.
Majaliwa alisema hayo Unguja Zanzibar alipozungumza katika ufunguzi wa maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani.
Alisema Kiswahili si kwamba ni lugha ya kitaifa tu kwa Watanzania bali ni fursa ya kiuchumi ambayo wanapaswa kuitumia vizuri.
“Niwaagize mawaziri wote wenye dhamana na lugha ya Kiswahili nawaona hapa waziri wa utamaduni bara na Zanzibar, waziri wa elimu pande zote mbili, Ofisi ya Rais Tamisemi ambayo ndiyo inashughulikia na inasimamia ufundishaji kwamba ni muhimu sasa kuweka mkakati ulio wazi kabisa wa kukuza Kiswahili katika shule na kuweka motisha za wale wote wanaofanya vizuri ili kuvutia wengi kushiriki,” alisema Majaliwa.
Majaliwa aliwaagiza Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Vijana na Waziri katika Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Sera na Uratibu na Baraza la Wawakilishi kuhakikisha kuwa wanaandaa mpango wa kutafuta ajira za kufundisha Kiswahili kwenye nchi mbalimbali ili Watanzania waende wakafanye kazi hizo.
Majaliwa alisema Kiswahili ni lugha inayotumika katika mawasiliano na kinazungumzwa duniani kote na kufundishwa katika vyuo vikuu duniani.
Aidha, alilishukuru Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) kwa uamuzi wa kuifanya Julai 7 kila mwaka kuwa maadhimisho ya Siku ya Kiswahili Duniani. Uamuzi huo ulitangazwa kupitia mkutano wa 41 wa Unesco wa Novemba 23, 2021.
Imeandikwa na Anna Mwikola (Dar es Salaam) na Mwandishi Wetu (Zanzibar).