Majaliwa mgeni rasmi siku ya malaria

WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa kesho anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho ya siku ya malaria duniani katika viwanja vya Mnazi Mmoja jijini Dar es Saalaam.
Kaimu Meneja wa Mpango wa Taifa wa Kudhibiti na Kutokomeza Malaria, Dk Abdalah Losasi alisema lengo la maadhimisho hayo ni kutoa elimu na hamasa zaidi kwa jamii juu ya kijikinga.
“Wakiweza kujikinga wataepuka madhara yanayatokana na ugonjwa huo na hatimaye tuweze kwa pamoja kuutokomeza kabisa hapa nchini ifikapo mwaka 2030,”alisisitiza Dk Losasi.
Akizungumza mwishoni mwa wiki hii katika semina ya waandishi wa habari jijini Dar es Salaam alisema vifo vitokanavyo na malaria vimeshuka kwa asilimia 76 kutoka vifo 6,311 vya mwaka 2015 hadi vifo 1,502 kwa mwaka 2022 huku waliothibitishwa kuwa na malaria wakipungua kutoka watu milioni 7.7 kwa mwaka 2015 hadi watu milioni 3.5 kwa mwaka 2022.
Aidha alisema kiwango cha maambukizi ya malaria kimepungua nchi ambapo mwaka 2008 takwimu zilionesha kuwa asilimia 18.1 walikuwa na malaria ikilinganishwa na takwimu za mwaka 2022 ambapo kiwango kilikuwa 8.1.
Alisema awali ni mikoa sita tu ilifanikisha kushusha kiwango cha malaria lakini sasa mikoa mitatu ya Songwe,Dar es Salaam na Mwanza yamefanikiwa pia na kufanya idadi kufikia tisa.
Dk Losasi anaeleza kuwa maeneo ya Vijijini yanamaambukizi makubwa kwa asilimia 10.7 ilikinganishwa na maeneo ya mjini ambayo ni asilimia 0.7.
Dk Losasi anabainisha kuwa watu wenye hali duni ya maisha wanakumbwa zaidi na malaria kwa asilimia 14.5 huku watu wanaoishi katika makazi bora kwa asilimia 0.6.