“MAONESHO ya kimataifa ya Afrika Mashariki ni muhimu sana kwa ajili ya sekta ya viwanda, lakini zaidi tunafurahi kwamba maonesho hayo yamefana sana mwaka huu, kwa sababu nchi nyingi zimeshiriki, ingawa India ndio wamejitokeza zaidi,” hiyo ni kauli ya Naibu Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Exaud Kigahe.
Ametoa kauli hiyo katika ufunguzi wa maonesho ya 23 ya biashara na viwanda yaliyoanza Alhamis jijini Dar es Salaam.
Amesema maonesho hayo yana umuhimu, kwani yatasaidia kujifunza teknolojia mbalimbali zinazotumiwa na nchi zilizoendelea.
“Katika maonesho haya tumekubaliana zaidi tutembelee na tuone jinsi wenzetu, ambao wameendelea zaidi kwenye teknolojia mbalimbali za viwanda wanavyoendeleza viwanda vyao,” alisema Kigahe.
Pia alisema kitendo cha maonesho hayo kufanyika nchini Tanzania, kitasaidia kukuza uwekezaji nchini.
“Tunajua awamu hii ya sita imesema waziwazi kwamba tunataka tuone sekta binafsi inakua, ndiyo sekta kiongozi katika kuleta mapinduzi ya viwanda na tunadhani inabidi tuweke mazingira mazuri ya uchumi wa viwanda kwa kuboresha mazingira wezeshi ikiwemo barabara, nishati, umeme, na usafirishaji na kuhamasisha upatikanaji wa malighafi katika eneo au sekta ya kilimo,” alisema Naibu Waziri huyo na kuongeza kuwa:
“Mwaka huu kwa mara ya kwanza tunaona mazao ya chakula na mazao ya biashara yamepata faida kubwa kwa sababu ya changamoto ya mazingira duniani, hivyo tunataka viwanda vinavyokuja viwe vinaendana na mabadiliko ya tabia ya nchi lakini pia visichafue mazingira.”
Comments are closed.