Marufuku watoto kupelekwa vibanda vya video

KAMANDA wa Polisi Mkoa wa Shinyanga, Janeth  Magomi amepiga marufuku watoto wadogo kuanzia umri wa miaka mitatu  hadi minane kupelekwa kwenye  vibanda vya kuonesha video katika msimu wa Sikukuu ya Pasaka.

Akizungumza na HabariLEO jana alisema baadhi ya  mabanda ya video yamekuwa  yakionesha video ambazo hazina maadili kwenye jamii.

Kamanda Magomi alisema lengo la kupiga marufuku  watoto wasiende kwenye vibanda vya video  ni watoto kuanza kujifunza vitendo viovu katika umri mdogo.

Advertisement

“Ulinzi na usalama kwa watoto  ni muhimu inatakiwa wazazi na walezi kukomesha vitendo viovu kwa kuanzia kwenye ulinzi wa mtoto na kile anachojifunza,”alisema.

Kamanda Magomi alisema jeshi la polisi limeimarisha ulinzi kuanzia kipindi chote cha Sikukuu ya Pasaka kuhakikisha watoto wahazururi hovyo na kwenda kwenye mabanda ya video.

Mwanasheria  Felix Ngaiza kutoka shirika la kupinga Vitendo vya Ukatili Aids Control Programu  (Agape) lililopo wilayani Shinyanga   alisema suala la ulinzi na usalama kwa watoto linahitaji umakini mkubwa kwa kushirikiana na wamiliki wa mabanda hayo wazazi  na vyombo vya usalama.

Ngaiza alisema ipo sheria ya mtoto ya mwaka 2009 namba 21 lengo lake mtoto  kuwa katika mazingira ya Ulinzi na kubaki akiwa  salama.

Mwenyekiti wa Mtaa wa Mitimirefu, Nassor Warioba  alisema wako tayari kushirikiana na jeshi la polisi  katika msimu huu wa sikukuu ya Pasaka kuwalinda watoto dhidi ya vibanda vinavyoonesha video  zisizo na maadili ni njia mojawapo ya kuharibu watoto.

Baadhi ya wazazi manispaa ya Shinyanga Joramu Musa na Selina Rugobi walisema vibanda vya kuonesha video vipigwe marufuku na kuhoji video zinazooneshwa  zinahakikiwa na nani na watoto wanapenda kuangalia ili mradi video imewekwa.

/* */