Mataifa 11 yajadili ubunifu kidijitali

MATAIFA 11 zimekutana Tanzania kwa ajili ya kubadilishana uzoefu wa jinsi ya kuwasaidia wabunifu wa kidijitali walioko katika nchi hizo.

Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), Dk Amos Nungu amesema hayo muda mfupi baada ya kufungua warsha ya wakufunzi wa wabunifu wa kidijitali katika nchi hizo zikiwemo Tanzania, Uganda na Nigeria.

Dk Nungu amesema katika kufanikisha hilo wakufunzi kutoka katika nchi hizo wataandaa mitaala ambapo COSTECH itasimamia jambo hilo.

Advertisement

“Ukumbi wa ubunifu wa Buni Hub kutoka Costech wakishirikiana na kumbi nyingine za ubunifu kutoka mataifa 11 wanaandaa masomo kwa ajili ya kufundisha vijana kwenye masuala ya ubunifu wa kidijitali,” amesema.

Amesema Mradi wa AfriConEU unafadhiliwa na Umoja wa Ulaya ambapo ukumbi wa Buni kwa kushirikiana na kumbi nyingine za ubunifu kutoka mataifa hayo 11 wameungana kuandika andiko la kujengea uwezo vijana wabunifu wa kidijitali.

Amesema vijana wengi wabunifu wana uwezo wa kuwa na bunifu nzuri ila changamoto wanayokutana nayo ni namna ya kufikia uwekezaji.

Mkufunzi Kutoka Taasisi ya Ubunifu ya Kibo Tanzania, Adam Kayoka amesema wanafundisha vijana teknolojia ya habari na mawasiliano hivyo kupitia mafunzo hayo wataimarisha zaidi ufundishaji wao.

” Kwa sasa hivi vijana wengi wanachangamkia fursa za kidijitali shida kubwa ipo kwenye ujuzi. Hivyo hapa tunajifunza namna nzuri ya kuwawezesha vijana kuzifikia hizo fursa na kuzitumia kwa usahihi zaidi,” amesema.

Kwa upande wake Meneja Mradi huo, Jose Gonzalez amesema Umoja wa Ulaya umefadhili Euro milioni 2 kwa ajili ya ukuaji wa kumbi bunifu za kijitali barani Afrika.

5 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *