Mavunde: GST imeiheshimisha sekta ya Madini

DAR ES SALAAM: TAASISI ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) imeiwezesha sekta ya madini kupiga hatua kiuchumi ikiwemo kuchangia asilimia 56 ya thamani ya bidhaa za madini zilizouzwa nje katika Mwaka wa Fedha 2022/23.

Hayo yamesemwa na Waziri wa Madini Anthony Mavunde jijini Dar es Salaam katika kikao cha wadau wa madini zikiwemo taasisi ya umma na binafsi zinazojishughulisha na Sekta ya Fedha chini ya Mwamvuli wa Umoja wa Mabenki Tanzania (TBA).

Amesema, sekta ya madini imechangia kodi za ndani kwa asilimia 15 ambazo ni sawa na Sh trilioni 2 pamoja na kuchangia Dola za Marekani Sh Bilioni 3.3. kutokana na mauzo ya bidhaa zinazotokana na rasilimali madini.

Advertisement

Mavunde amesema, wizara itawezesha kufanyika kwa utafiti wa angalau kufikia asilimia 50 ifikiapo mwaka 2030 kwa ushirikiano wa taasisi hizo, tafiti hizo zitaliwezesha taifa kupiga hatua kubwa zaidi za kimaendeleo na kiuchumi kupitia Sekta ya Madini.

‘’Tunataka kufahamu taarifa za miamba, ili tupime vizuri, hii ndiyo sababu ya dira ya 2030;…“ “Ikifika 2030 tuwe tumefanya utafiti kwa nchi yetu kwa angalau asilimia 50.”Amesema

Aidha, amesema pamoja na mafanikio hayo bado mchango wa sekta ya madini haujakidhi matarajio ya watanzania na taifa.

“Zipo changamoto ndiyo sababu tumekutana kupitia kikao hiki kujadili kuwaonesha kilichopo kwenye sekta ya madini, changamoto zilizopo na kutuondoa tulipo,’’ amesema.

Akizungumzia Madini ni Maisha na utajiri amesema haviwezi kutenganishwa na maisha ya mtanzania na Sekta ya Madini na kueleza kuwa kufanikiwa kwa tafiti za kina na kupatikana kwa taarifa za awali, zitachochea sekta nyingine kukua ikiwemo Sekta ya maji na kilimo.

“Kilimo wana mkakati wa kuchimba mabwawa 100, kupitia taarifa za GST inaweza kujulikana aina ya maji na hivyo kufanya kilimo chake kwa tija na kuwezesha usalama wa chakula na mapato.

Amesema sekta ya madini inaweza kuokoa matumizi ya fedha za kigeni kwa kununua mbolea kutoka nje.

“Zaidi ya tani 350,000 za mbolea zinaagizwa nje kwa kutumia fedha za kigeni kwa ajili ya matumizi ya kupandia, kukuzia na kustawisha , hivyo, taarifa za miamba zitasaidia kujua miamba yenye malighafi zenye mbolea inayohitajika na hivyo kusaidia shughuli za kilimo chenye tija,”amesema Mavunde.

Aidha, amesema GST imewahi kufanya utafiti wa kina mwaka 2004 kwa kurushwa ndege katika maeneo ya Kahama, Biharamulo, Nachingwea na Mpanda kwa ukubwa wa kilomita za mraba 30,000 ikilinganishwa na eneo la ukubwa wa nchi ya Tanzania yenye ukubwa wa kilomita za mraba 945,000 ni kiasi kidogo sana.

“Ndiyo sababu tumekutana na ninyi tuwaeleze fursa ziizopo kwenye Sekta ya Madini ,tushirikiane,’’ amesema Waziri Mavunde.

9 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *