Mavunde kuandaa tuzo za wajasiriamali

MBUNGE wa Jimbo la Dodoma Mjini Anthony Mavunde ameanzisha tuzo maalum ya wajasiriamali ambayo italenga kuongeza wigo wa uchakataji bidhaa za kilimo na mifugo.
Kikundi kitakachoibuka kidedea katika tuzo hizo zitakazosimamiwa na Sido kitapatiwa mitambo na mashine ndogo zenye thamani ya sh milion 20.

Mavunde ameyasema hayo katika viwanja vya Nyerere Square wakati akifunga mafunzo ya wajasiriamali mkoani Dodoma chini ya mwavuli wa Taasisi ya Wanawake na Uchumi wa Viwanda(WAUVI).

“Ninawapongeza sana WAUVI kwa mafunzo hayo yenye lengo la kuwajengea uwezo wajasiriamali wa Dodoma ili kuongeza thamani ya bidhaa wanazozalisha.” Amesema na kuongeza
“Ninaona jitihada kubwa sana za wajasiriamali hapa Jijini Dodoma ambao naamini tukiwasaidia kwa kuwaongezea mtaji na mashine za kisasa wanaweza kupiga hatua na kuleta mapinduzi makubwa.” Amesema
Aidha, amesema anamshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutengeneza fursa zaidi za kiuchumi kupitia uwekezaji mkubwa unaoendelea wa kuijenga Makao Makuu Dodoma.

Awali akizungumza Mwenyekiti wa WAUVI Taifa Rehema Mbeleke amesema mafunzo hayo kwa wajasiriamali 3000 yana lengo ya kuwajengea uwezo ili kushiriki katika masoko ya ushindani wa bidhaa.



