MBUNGE wa Jimbo la Korogwe Vijijini, Timotheo Mzava, amekabidhi mabati 100, saruji mifuko 100 pamoja na tofali 1500 kwa ajili ya kuanzisha ujenzi wa shule mpya ya sekondari katika Kata ya Magoma.
Akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Kijiji cha Kwamazandu, Kata ya Magoma, amesema kuwa changamoto ya umbali imemgusa na hivyo kuamua kutoa msaada huo, ili ujenzi wa shule uweze kuanza mara moja kwa nguvu za wananchi.
” Wanafunzi katika Kata hii wanalazimika kutembea umbali mrefu kwenda shule pamoja na kurudi, jambo ambalo limesababisha wanafunzi wengi hususani wa kike kukutana na changamoto mbalimbali zinazopelekea baadhi yao kukatisha masomo,”amesema Mzava.
Amesema kuwa kila mwaka kuna wanafunzi zaidi ya 120 kutoka katika shule za msingi za Kwamazandu, pamoja na Makorora hivyo wanatosha kuanzisha shule nyengine ya sekondari kwenye kata hii kwa upande huu kuwasaidia watoto wetu,” amesema.
Amesema kuwa lengo ni kuhakikisha wajenga shule ya sekondari kwenye kata hiyo ya kisasa, ili kusaidia wanafunzi wa shule hizo mbili za msingi kuweza kupata shule ya sekondari, hivyo malengo yao ni kukamilisha shule hiyo inakamilika mapema mwaka 2025 na kuwasaidia watoto hao kupata elimu yao kwenye mazingira ya karibu.