Mhariri HabariLEO ashinda tuzo ya Mwalimu Nyerere

MHARIRI wa gazeti la serikali la HabariLeo, Hamisi Kibari, ameshinda tuzo ya ubunifu ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu katika nyanja ya Riwaya.
Tuzo hiyo imetolewa usiku wa kuamkia leo na Rais Mstaafu wa Msumbiji, Joachimu Chisano, jijini Dar es Salaam.
Kibari ameshinda kupitia riwaya yake ya ‘Gereza la Kifo’ ambapo amezawadiwa shilingi millioni 10, Ngao ,Cheti na kuchapishiwa mswaada wake “Gereza la Kifo’ ambao pia utasambazwa mashuleni.
Mshindi huyo ni mtunzi wa riwaya, mashairi na mtengeneza filamu. Kwa kipindi cha takribani miaka 20, amekuwa akiandika hadithi katika magazeti mbalimbali nchini Tanzania na baadhi kutumika katika filamu.
Kitaaluma, ni mwalimu na mwandishi wa habari mkongwe nchini Tanzania ambaye ana shahada ya sanaa (BA-Education) ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na sasa anamalizia shahada ya pili katika Mawasilino ya Umma ya Chuo Kikuu Huria cha Tanzania (OUT).
Hata hivyo, Kibari hakuwepo kwenye hafla hiyo ya tuzo na badala yake tuzo yake ilipokelewa na Mwandishi Mwandamizi wa HabariLeo Joseph Sabinus kwa niaba.
Aidha, mshindi wa kwanza katika upande wa ushahiri ameshinda Amri Rajabu Abdalah kupitia kitabu chake cha ‘Mtale wa Ngariba’.
Rajabu nae pia amezawadiwa shilingi Milioni 10 , Ngao, Cheti na kuchapishiwa mswaada wake na kusambazwa mashuleni.
Mshindi huyo alihitimu kidato cha sita katika shule ya Sekondarai Shambalai iliyopo Tanga na baadae kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na kuhitimu shahada ya Sanaa na Elimu (B. A Ed) kwa masomo ya Kiingereza na Kiswahili mwaka 2016.