Mikakati kudhibiti athari za mitandao kwa watoto yaja

DAR ES SALAAM: Serikali kupitia wizara ya maendeleo ya jamii imewataka wazazi kuhakikisha wanasimamia maadili ya watoto ikiwemo kudhibiti watoto kujihusisha na mitandao ya kijamii kufuatia mitandao hiyo kuathiri zaidi ya asilimia 5 ya watoto kati ya watoto asilimia 67 wanaotumia mitandao ya kijamiii.

Akizungumza leo Waziri wa maendeleo ya jamii, Dorothy Gwajima wakati wa kufungua kikao na wadau wa vyombo vya habari wakati wa semina ya wadau hao juu ya masuala ya usalama mtandaoni dhidi ya watoto.

Waziri Gwajima amesema kati ya watoto asilimia 67 ya wanaojihusisha na mitandao asilimia 4 ya watoto wamebainika kujihusisha na mitandao maarufu ikiwemo Facebook, Instagram, twitter na telegram.

Advertisement

Pia, Gwajima amesema kutokana na ongezeko hilo la watoto katika mitandao na athari zinazo tokana na mitandao serikali imeamua kuja na mkakati ili kukabiliana na athari hizo ambazo zinatajwa kupelekea watoto kujihusisha na ngono wakiwa na umri mdogo.

Kwa upande mwingine, Mtaalamu wa masuala ya kimtandao na Mchunguzi wa makosa ya kidijitali Yusuph Kileo, amesema kwa mujibu wa tafiti kati ya watoto wa miaka 8 hadi 10 wanatumia masaa nane kwenye mitandao ya kijamii jambo ambalo sio jema na kutoa wito Kwa jamii kuwa karibu na watoto pindi wanapotumia mitandao ikiwa ni pamoja na kuwapa elimu juu ya faida na madhara yake.

Pia,Afisa ulinzi wa mtoto kutoka shirika la watoto UNICEF, Joseph Matimbwi ,amesema lengo la kampeni hii ni kuwajengea uwezo watoto wenyewe kuelewa juu ya ukatili wa kimtandao kwani tayari wengi wameshaathirika na ukatili huo.

Hata hivyo serikali imeendelea kusisitiza wazazi kutumia nafasi zao kuhakikisha wanawasaidia watoto hasa umri wa miaka 12 hadi 17 kujiepusha na matumizi mabaya ya mitandao ya kijamiii ambayo imekuwa ikileta athari kubwa kwa watoto.