Mitaala urekebishaji tabia kwa wafungwa kuandaliwa

JESHI la Magereza imeanza kazi ya uboreshaji  wa mitaala ya urekebu  kwa  wafungwa ikiwa ni utekelezaji wa  maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan pamoja na mapendekezo ya tume aliyoundwa kwa ajili ya maboresho ya vyombo vya utoaji  haki jinai nchini.

Hatua hiyo imefikiwa  ili  kuboresha baadhi ya maeneo  yaliyoonekana kuwa na mapungufu ambayo yanachangia kwa namna moja ama nyingine  waharifu kurudia makosa yao wanapokuwa uraiani.

Kamishna Jenerali wa Jeshi hilo Ramadhani Nyamka alisema hayo mjini Morogoro wakati alipozindua  kazi ya uandaaji mitaala ya Urekebishaji tabia  kwa wafungwa kuanzia ngazi ya astashahada  na shahada.

Advertisement

Mitaala hiyo mipya itatumika kufundishia Maofisa wa  Magereza na Askari kwenye Vyuo vyake ili  na wao waweze kwenda kutoa mafunzo yanayostahiki ya urekebu kwa wafungwa magerezani .

“ Mheshimiwa Rais alilitaka jeshi letu  la Magereza  kuhakikisha taratibu au program za urekebu kwa waharifu zinafanyika kwa kiwango stahiki na kinachokubalika” alisema Kamishna Jenerali Nyamka.

Nyamka, alisema hata  mapendekezo ya Tume ya Rais aliyoiunda kwa ajili ya maboresho ya vyombo vya haki jinai , moja ya mapendekezo yake yaliitaka Jeshi la Magereza liboreshe mitaala yake na lengo nikuwa kuwa na program za urekebishaji.

Alisema , mitaala hiyo inayohuiswa itaweza kuwarekebisha wafungwa wanaoingia gerezani, wamalizapo vifungo vyao na kurudi uraiani kuijunga na watanzania wengine katika shunguli za ujenzi wa uchumi  wa Taifa  ili waonekane wamerekebika.

Kamishna Jenerali wa Jeshi hilo , alisema kazi ya urekebishaji waharifu ni kazi ya kitaalam, hivyo inahitaji miongozo na mitaala inayoakisi hali ya sasa na inayoendana na wakati.

Alisema , mapitio ya mitaala , mafunzo sahihi kwa maofisa wa magereza na askari  katika tasnia ya urekebu yanatakiwa kupewa uzito unaostahili  ndani ya jeshi hilo.

“ Moja ya kielelezo cha kuonesha wamerekebika ni  kuodokana na tabia ya urudiaji wa kutenda makosa ambayo yanawarudisha tena gerezani. “ alisema Nyamka.

“  Kwa sasa tumeona turekebishe mitaala kwa kushirikiana na Nactvet ,Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima  Mamakala ya Mafunzo ya Ufundi Stadi (Veta) na timu ya wataalamu wa magereza kwa kukaa pamoja ili waje na mitaala ambayo imejitoshereza.” alisema Nyamka.

Kamishna Jenerali Nyamka ,alisema licha ya  maboresho ya mitaala, jamii ina jukumu kubwa la kuwasaidia wafungwa wanaomaliza vifungo vyao ambao  tayari wanakuwa  ujuzi  ili waweze kujitegemea kiuchumi na sio kuwanyanyapaa.

“ Wakati  mwingine mfungwa anapotoka gerezani  kwa kutumia programu za  urekebu gerezani,  amekuwa na  taaluma ama ujuzi ambao alipoingia   hakuwa nao, anapotoka  ni fundi seremala mzuri, jamii iwe na utayari kuwasaidia” alisema

Nyamka ,alishauri  jamii iwasaidie  watu hao wenye ujuzi vitendea kazi ambapo nni njia bora ya kumtengenezea mazingira ya kuendeleza ujuzi wake na kuweza kudumu maisha ya kila siku na kufanya  tatizo la urudiaji wa makosa  ufumbuzi wa kudumu .

“  Jamii kwa upande mmoja iwe tayari kuwasaidi na kwa upande wapili Jeshi la Magereza lenyewe litaendelea kuboresha mitaala na kwamba tatizo hilo litakuwa limekwisha kabisa” alisema Nyamka.

Naye  Kaimu Meneja wa Ukuzaji Mitaala, Utafiti na Upembuzi Yakinifu kwa Soko  wa Baraza la Taifa na Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET), Dk  Magreth Shawa alilipongeza Jeshi hilo kwa kufuata taratibu na miongozo ambayo  imewekwa na Baraza .

Miongozo hiyo ni pamoja na  kuhuisha mitaala ili iendane na kuzalisha watu wanaoweza kuajirika kwenye Magereza na kufanya kazi ambazo ni za kurekebisha wafungwa ili  wanaomaliza vifungo vyao waweze kujitegemea na kutokurudia makosa.

“ Mitaala inakuwa na sehemu tatu, inarekebisha akili ya mtu, inarekebisha mikono ya mtu jinsi ya kutenda na inarekebisha mtizamo lazima abadilike” alisema Dk Shawa.

Dk Shawa, alisema kama  ilivyo  sasa wengi wa wafungwa wakitoka gerezani  na kwenda kwenye jamii ,watu wanawaogopa wanawanyanyapaa ,lakini tunataka wakitoka huo  mtaala uwe umewasaidia kiujuzi ili wasirudie tena makosa wakiwa uraiani.

8 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *