Mkakati wa kukomesha habari za upotoshaji waja

WAZIRI wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye.

SERIKALI imeazimia kuharakisha kuzindua mkakati wa kitaifa wa mawasiliano nchini.

Hatua hiyo inalenga kuhakikisha kuwa taarifa na ujumbe muhimu unatoka na kuwasilishwa kutokana na vyanzo vya kuaminika.

Hayo yalibainishwa jana na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye na kuongeza kuwa lengo la hatua hiyo pia ni kukomesha habari za upotoshaji na kupiga vita habari za uongo bila kuingilia uhuru wa kujieleza.

Advertisement

Nape alikuwa akiulizwa maswali na waandishi wa habari baada ya kuhitimisha mafunzo ya watendaji wakuu wa wizara hiyo na kusisitiza kuwa serikali itaharakisha mkakati huo kwa lengo la kuchuja idadi ya wasemaji na watoa taarifa.

“Mara nyingi tumejikuta tukiingia kwenye mlolongo wa kauli na ufafanuzi kutoka kwa watu wanaodai ni watoa taarifa, hasa wakati wa majanga na matatizo mengine… tunataka kukamilisha mkakati huu mwaka wa fedha ikiwa katika hatua ya juu,” alisema.

Kwa mujibu wa Nape mkakati huo wa kitaifa utawawezesha Watanzania kusoma taarifa sahihi na sio suala la mikakati ya uwazi wa mawasiliano lakini kuzipata kwa wakati bali pia kuboresha upatikanaji wa habari kutoka kwa vyanzo vinavyoaminika.

“Jukumu letu litakuwa ni kuhakikisha kuwa taarifa muhimu zinawasilishwa kwa watu sahihi, kupitia mawasiliano ya ndani na nje,” alisema.

Nape alisisitiza pia kuwa serikali imejizatiti kutatua changamoto za mawasiliano ili kuhakikisha kuwa kuna mawasiliano ya uhakika miongoni mwa Watanzania, utoaji huduma bora za mawasiliano na nafuu kwa wananchi.

Alisema vilevile wizara yake itajitahidi kuyafanya mashirika na taasisi zake zinafanya kazi kwa ufanisi na alidokeza hatua ambazo serikali imebainisha kuyanusuru.

“Tayari tumemaliza deni kubwa ambalo Shirika la Posta Tanzania lilikuwa likikabiliana nalo, lakini tunafurahi kwamba sasa limeanza kufanya kazi,” alisema na kutaja hatua nyingine kuwa ni pamoja na kuzindua Shirika la Mawasiliano Tanzania (TTCL).

Wizara na watendaji wake walikutana jijini Arusha kwa ajili ya mafunzo ya siku tatu kutathmini sekta hiyo ilipotoka na inakoelekea.

2 comments

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *