Mkurugenzi Jatu afutiwa kesi, akamatwa tena

MKURUGENZI Mtendaji wa Kampuni ya JATU Plc, Peter Gasaya amekamatwa tena saa chache tu baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP) kumfutia kesi ya kujipatia Sh bilioni 5.1 kwa njia ya udanganyifu.
DPP aliwasiliasha mapema leo Aprili 11, 2023 hati ya kutokuwa na nia ya kuendelea na kesi hiyo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu chini ya kifungu namba 91 (1) cha Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai.
Muda mchache baadaye, Gasaya akiwa bado yuko Kisutu aliwekwa chini ya ulinzi na kupandishwa mahakamani ambapo alisomewa kesi ya Uhujumu uchumi yenye mashtaka mawili; kujipatia fedha kiasi cha Sh bilioni 5.1 na kutakatisha fedha.
Gasaya amesomewa mashtaka mapya na Wakili wa Serikali, Adolf Verandumi mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Pamela Mazengo.