Mkurugenzi Jatu ashindwa masharti ya dhamana

Mkurugenzi Jatu ashindwa masharti ya dhamana

MSHITAKIWA Peter Gasaya (32), ambaye ni Mkurugezi Mtendaji wa Kampuni ya Jatu Public limited  anayekabiliwa na shitaka la  kujipatia fedha tasilimu Sh 5,139,865,733.00 kwa njia ya udanganyifu, amefikishwa  Mahakama ya Hakimu Mkazi  Kisutu, Dar es Salaam kwa ajili ya kupewa masharti ya dhamana.

Wakili wa serikali Tumaini Maingu alieleza mahakama leo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Mery Mrio anayeisikiliza kesi hiyo, ambapo alidai kuwa kesi hiyo imeitwa kwa ajili ya mshitakiwa kupewa masharti ya dhamana, baada ya siku nne kupita tangu alipofikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza akikabiliwa na shitaka hilo.

Baada ya kusikiliza maombi hayo Hakimu Mrio alitoa masharii matatu dhidi ya mshitakiwa huyo, ambapo alitakiwa kuwasilisha fedha taslimu Sh 2,600,000,000 au hati ya  mali isiyohamishika yenye thamani hiyo.

Advertisement

Pia alitakiwa awe na  wadhamini wawili wanaotambuliwa kisheria ambao watakuwa na barua kutoka serikali za mtaa, ikiwa imeambatanishwa na  kitambulisho cha Taifa au  cha mpiga na  wawe wakazi wa  Dar es Salaam.

” Wadhamini hawa wanatakiwa kusaini nusu ya mali iliyotajwa kwenye hati ya mashtaka au kuwasilisha hati ya mali yenye thamani ya Sh 2,600,000,000 na hati hiyo itabidi ihakikiwe kwanza kabla ya kuletwa mahakamani hapa,” alisema Mrio.

Hata hivyo mshtakiwa ameshindwa kutimiza masharti hayo na  kurudishwa rumande hadi Januari 11, 2023 kesi hiyo itakaporudi kwa ajili ya kutajwa.

Kwa mujibu wa hati ya mashitaka inadaiwa kuwa katika terehe isiyofahamika kati ya Januari mosi  na  Desemba 31, mwaka 2021 ndani ya mkoa wa Dar es salaam Mshitakiwa akiwa  Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Jatu Public Limited, alijipatia Sh 5,139,865,733.00 kutoka  Saccos  ya Jatu akijinasibu kukizalisha  kiasi hicho cha fedha kwa kuwekeza fedha katika kilimo cha faida wakati akijua  si kweli.

Mshitakiwa alipandishwa kizimbani Desemba 29, mwaka 2022 akikabiliwa na shitaka la kujipatia fedha tasilimu shilingi 5,139,865,733.00 kwa njia ya udanganyifu.

 

Add a comment

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *