CCM Moro wakomaa na vigogo uharibifu wa mazingira

CCM Moro wakomaa na vigogo uharibifu wa mazingira

CHAMA cha Mapinduzi (CCM, Wilaya ya Morogoro kimemuomba Waziri wa Maji, Jumaa Aweso kufikisha kilio cha wananchi kwa  Rais  Dk Samia Suluhu Hassan kuhusu mawaziri watano wanaodaiwa kumiliki idadi kubwa ya mifugo, ili waiondoe  kunusuru uharibifu wa mazingira na  vyanzo vya maji vinavyosaidia mikoa ya Dar es Salaam, Pwani na  Morogoro.

Mwenyekiti CCM wa Wilaya hiyo , Gerold Mlenge alitoa ombi hiyo kwa  Waziri Aweso  Januari 4, 2023 kwa niaba ya wananchi alipofanya ziara ya kutembelea, kukagua na kuzindua ujenzi wa miundombinu ya mradi wa maji katika Kata ya  Lundi, Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro.

Mlenge amesema  kwa asili yake  halmashauri ya  Morogoro haina eneo la ufagaji bali ni ya kilimo cha mazao mbalimbali, lakini kwa sasa  wafugaji wengi wavamizi maeneo ya ardhi inayotumika kwa kilimo  na mifugo hiyo kukaharibu mazingira na vyanzo vya maji  ikiwa pamoja na kusababisha migogoro baina ya wafugaji  na wakulima.

Advertisement

“ Uwepo wa wingi wa mifugo umedhihirisha kuharibu vyanzo vya maji na kusababisha kuwepo kwa migogoro baina ya  wakulima na wafugaji inayotokana na kugombea matumizi ya ardhi na kwa  ujumla jambo hili  linaweza kupatiwa ufumbuzi,” amesema Mlenge.

Alimuomba Waziri Aweso kuyachukua  majina ya mawaziri hao kutoka kwa Mkuu wa Wilaya ya Morogoro, ambaye alifikishiwa taarifa na majina hayo ambaye aliahidi  kuyafanyia kazi.

“Isifike mahali nikaita press ( mkutano na waandishi wa  habari ) nikawataja kwa majina, naomba muende  mkanong’onezane watoe mifugo yao huku Morogoro vijijini hatuna asili ya mifugo, sisi kazi yetu ni kulima, hatutaki migogoro, hatutaki migogoro ya wakulima na wafugaji,” anasema Mlenge.

Naye Chifu Kingalu wa Waluguru Mwanabanzi wa 15, amesema  Mkoa wa Morogoro ni mkoa wa kimkakati  katika chakula, miundombinu barabara  na upatikanaji wa maji kwa ajili ya uzalishaji wa umeme.

Kutokana na hali hiyo amekerwa na tabia za baadhi ya viongozi wa serikali waliopewa dhamana wakiwemo mawaziri kufanya shughuli za ufugaji katika sehemu za vyanzo vya maji.

“ Ng’ombe zilizopo ukanda wa Morogoro Kusini sio za wananchi wa maeneo hayo, bali ni za baadhi ya mawaziri wenzako, viongozi wa serikali na wakuu wa idara ambao wanajulikana …kwa nini zisiondoshwe hizo ng’ombe, “ alisema Chifu Kingalu.

Kwa upande wake Waziri Aweso akizungumza na wananchi wa  kijiji cha Lundi amesema , changamoto ya uhaba ama ukosefu wa maji  ni kutokana na kuharibiwa kwa vyanzo vyake mara kwa mara kunakosabishwa na suala la mifugo.

Waziri Aweso amewaahidi wananchi hao kuliwasilisha bila kukosa kwa Rais Dk Samia lalamiko lao juu ya mawaziri watano, wanaodaiwa kumiliki mifugo mingi wilayani humo.

“Mmenipa ombi maalum na viongozi wa chama wa  wilaya hii  juu ya changamoto ya mifugo, nikiri kulipokea na nitalipeleka kama lilivyo kama mlivyotaka, mimi ni muathirika pia,” amesema  Aweso

/* */