Mradi wa maji kunufaisha 4,604 Ng’ongola, Lundi

WAZIRI wa Maji , Jumaa Aweso ameweka jiwe la msingi mradi wa maji Lundi, kata ya Lundi utakaowanufaisha wananchi wapatao 4,604 kutoka vitongoji saba vya Viijiji vya Ng’ongola na Lundi halmashauri ya Wilaya ya Morogoro.
Wananchi hao wanatarajia kupata maji safi na salama baada ya kujengwa mradi huo wenye kugharimu sh milioni 492.8 zilizotolewa na serikali.
Naye Meneja wa Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA), halmashauri ya wilaya hiyo Mhandisi Grace Lyimo, amesema hayo Januari 4, 2023 kuwa mradi huo ulianza kutekelezwa Januari 17, mwaka 2022 na ulitarajiwa kukamilika Julai 16, 2022.
Lakini kutokana na changamoto zilizojitokeza, mkandarasi ameongezwewa muda hadi ifikapo Februari 7, mwaka huu na kwamba chanzo cha maji cha mradi huo ni kisima kirefu chenye uwezo wa kuzalisha lita za ujazo 264,000 kwa siku, ambapo mahitaji ya maji katika vijiji viwili hivyo ni lita za ujazo 230,200 kwa siku.
Mhandisi Lyimo amesema utekelezaji wa kazi katika mradi huo umefikia asilimia 69 na kiasi cha Sh milioni 212. 5 kimeshalipwa kwa mkandarasi.
“ Mradi huu ukikamilika kwa asilimia 100 utatimiza azma ya serikali ya awamu ya sita ya kutoa huduma bora za maji safi na salama kwa wananchi wa vitongoji saba katika vijiji vya Ng’ongola na Lundi,” amesema Mhandisi Lyimo.