Msisitizo upimaji ardhi Bunge likipitisha bajeti ya Sh bil 171.4

Wizara kupima ardhi yote, migogoro basi

 BUNGE limeridhia makadirio ya mapato na matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ya Sh biliioni 171.4 kwa mwaka wa fedha 2023/24, huku Waziri Dk Angeline Mabula akisema Serikali imejipanga kupima ardhi yote ya nchi, ili kuondokana na migogoro inayoibuka katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Kabla ya kupitisha mpango huo, kilio kikubwa cha wabunge kilikuwa ni migogoro ya ardhi pamoja na mipaka ya vijiji pamoja na hifadhi.

Mbunge wa Mlimba, Godwin Kunambi alifikia kufika ‘kushika shilingi ya waziri’ akitaka maelezo zaidi juu ya mpango wa Serikali wa kupima ardhi. Hata hivyo Mbunge wa Nyasa, Mhandisi Stella Manyanya alimsihi Kunambi kuondoa hoja ili jambo hilo likajadiliwe kwenye Kamati ya Fedha kama alivyopendekeza Waziri Jenista Mhagama.

Advertisement

Miongoni mwa mambo sita ambayo Wizara imepanga kuyatekeleza katika mwaka ujao wa fedha, Dk Mabula ameliambia Bunge, Dodoma leo asubuhi kuwa ni kuimarisha mifumo ya utatuzi wa migogoro ya ardhi na kuongeza kasi ya upangaji, upimaji na umilikishaji wa ardhi.

Waziri amesema mambo mengine yanayotarajiwa kutekelezwa ni kuwekeza zaidi katika matumizi ya mifumo ya TEHAMA katika utunzaji wa, kumbukumbu, utoaji huduma na upatikanaji wa taarifa za ardhi pamoja na kuweka mazingira rafiki ya upatikanaji wa ardhi ya uwekezaji.

Wizara imepanga kuongeza ufanisi katika ukusanyaji wa maduhuli ya serikali yatokanayo na sekta ya ardhi ikiwa ni pamoja na matumizi ya teknolojia rahisi ya mawasiliano ya simu za mkononi; na kuimarisha mipaka ya kimataifa,” Waziri amelieleza Bunge.

Akichangia hotuba mara baada ya uwasilishaji wa hotuba ya Waziri, Mbunge wa Tarime Vijijini Mwita Waitara amemtaka Waziri kushughulikia migogo ya ardhi na fidia ya itolewe kulingana na thamani ya rasilimali.

Baadhi ya wabunge waliochangia hotuba hiyo baada ya Waitara wameitaka Wizara kupima ardhi yote ili kukabiliana na wingi wa migogoro ya ardhi hapa nchini.

Add a comment

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *