Kocha Mkuu wa Yanga, Nasreeden Nabi amesema bado inawezekana kwa timu hiyo kupata matokeo ugenini licha ya kupoteza kwa mabao 2-1 kwenye fainali ya kwanza iliyochezwa Uwanja wa Benjamini Mkapa, Dar es Salaam.
Kocha Nabi anasema kama jezi za wachezaji wake zitavuja jasho la mapambano basi inawezekana kupindua meza nchini Algeria.

Kwa upande wake kocha wa USM Alger Abdelhak Benchikh,a amesema vijana wake wamecheza soka safi ndio maana wamepata matokeo.
“Wachezaji wangu wamejitoa kupata matokeo haya, haikuwa rahisi kucheza kwenye mazingira haya ya uwanja,” amesema.
Yanga ikicheza mbele ya maelfu ya mashabiki waliojitokeza uwanjani, Yanga ilienda mapumziko ikiwa nyuma kwa bao 1-0 lililofungwa na Aymen Mahious dakika ya 32, kabla ya Fiston Mayele kusawazisha dakika ya 82.
Hata hivyo furaha za mashabiki wa Yanga hazikudumu kwani dakika ya 84 Islam Merili alifunga bao la pili na kuwapa wakati mgumu Watanzania waliokuwa uwanjani na waliokuwa wakifuatilia mchezo huo kwenye televisheni au mitandao ya kijamii.
Yanga sasa wanahitaji matokeo ya ushindi wenye faida kwao kwenye mchezo wa mkondo wa pili utakaopigwa Juni 3 nchini Algeria.
*Imeandaliwa na Antipas Kavishe, Frank Buliro na Ismaily Kawambwa.