MWANAFUNZI wa kidato cha tatu, Shule ya Sekondari Ally Mchumo, Tarafa ya Kipatimu, mkoani Lindi, Jamila Adamu (17), ameuawa kwa kuchomwa na kitu chenye ncha kali na watu waliovamia nyumba yao wakitaka wapewe fedha walizopokea kutoka Mfuko Maendeleo ya Jamii (TASAF).
Kwa mujibu wa taarifa zilizothibitishwa na viongozi wa Serikali ya Kijiji, Kata na Kamanda wa Polisi mkoani Lindi, Pili Mande, tukio hilo lilitokea Juni 30, mwaka huu.
Mwenyekiti wa Kijiji cha Chumo, Abdallah Ngomba, amesema, tukio hilo lilitokea baada ya vijana wawili kuvamia nyumbani kwa mama wa marehemu Jamila Manate Kikaka na kulazimisha wapewe fedha alizolipwa na TASAF.
Amesema siku ya tukio, Jamila na mama yake wakiwa ndani ya nyumba yao wamelala, vijana wawili aliowataja kwa majina, Nassoro Mailo na Abbasi Kapandaila, waliingia ndani mwao na kuanza kupekua wakitafuta fedha ndipo Jamila aliposhtuka kutoka usingizini na kupiga kelele za wezi.