MWENYEKITI wa Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF), Angelina Ngalula amesema biashara kati ya Tanzania na India inatarajiwa kufikia dola za Marekani bilioni sita mwaka huu.
Ngalula amesema hayo alipokutana na kufanya mazungumzo na Spika wa Bunge la India, Om Birla.
Amesema kufikiwa kwa kiwango hicho cha fedha, inatokana na kufunguliwa kwa masoko ya bidhaaa za kilimo ikiwepo parchichi na nafaka mbalimbali.
“ Kwa sasa Tanzania inanunua bidhaa zaidi ya tunavyouza kwenda India, ila tunawaalika wafanyabiashara kutoka India kuwekeza kwenye viwanda vitakavyoongeza thamani ili kuongeza biashara kupunguza tofauti hii.
“Na pia kuendelea kufungua masoko ya bidhaa za Tanzania kwenda India. India ndio soko kubwa la bidhaa za Tanzania,” amesema.
Pia amemshukuru Birla kwa niaba ya TPSF kwa kutenga muda wake kuitembelea Tanzania, kwani inaonesha uhusiano mzuri wa diplomasia na uchumi kati ya nchi hizi mbili.
Naye Spika huyo wa Bunge la India Birla, ameelezea umuhimu wa kuendelea kushirikiana kibiashara kwenye sekta za kilimo, afya, elimu, Tehama, viwanda pamoja na eneo la ukanda wa viwanda.