CHUO Kikuu Mzumbe (MU), kilichopo mkoani Morogoro,kimetengewa dola milioni 21 za Kimarekani kwa ajili kuboresha mazingira ya kufundishia na kuanzisha programu za Vyuo vikuu zinazoendana na mahitaji ya soko la ajira.
Fedha hizo zinatokana na Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi kwa Tanzania (HEET) unaofadhiliwa na Benki ya Dunia ukiwa ni mkopo kwa serikali ya Tanzania na unaratibiwa na Wizara ya Elimu , Sayansi na Teknolojia na unatekelezwa na Vyuo Vikuu pamoja na Taasisi zingine zilizopo chini ya wizara hiyo
Kaimu Mkuu wa Chuo kikuu hicho Profesa William Mwegoha amesema hayo Novemba 24, 2022 wakati akitoa taarifa kwa Mkuu wa chuo Kikuu hicho ambaye ni Rais Mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ,Dk Ali Mohamed Shein kwenye Mahafari ya 21 iliyofanyika kampasi kuu ya Morogoro.
Amesema lengo la mradi huo ni kuboresha mazingira ya kufubndishia na kuhakikisha kuwa program katika Vyuo Vikuu zinaendana na soko la ajira na Chuo hicho kimetengewa dola za kimarekani milioni 21 kwa ajili ya kutekeleza miradi hiyo.
Profesa Mwegoha amesema kuwa miradi inayotekelezwa na Chuo kikuu hicho kupitia mradi wa HEET ni ujenzi wa miundombinu ya kufundishia , ambapo miradi hii inachukua asilimia 79.2 ya fedha zote za mradi.
Ametaja mradi hiyo ni kupitia mitaala na kutengeneza mitaala mipya ili iendane na soko la ajira , kuboresha TEHEMA na miundombinu yake, kuboresha uhusiano wa chuo na wadau wa nje, kuwajengea uwezo wafanyakazi wa chuo pamoja na kuanzisha Kampasi mpya katika mkoa wa Tanga.