NAIBU Waziri wa Maliasili na Utalii, Mary Masanja amesema ili kuhakikisha vijana wengi wanalitumikia taifa, jeshi la uhifadhi wa wanyamapori na misitu imekuwa ikiajiri askari waliohitimu astashahada ya wanyamapori, misitu pamoja na askari waliohitimu Jeshi la kujenga taifa (JKT) kwa mkataba.
Akizungumza leo, Juni 20, 2023 bungeni, jijini Dodoma naibu waziri huyo amesema mkakati huo unalenga kutatua changamoto ya upungufu wa watumishi hususan askari.
“SUMA JKT wamekuwa wakiingia mikataba ambayo inawezesha vijana waliohitimu JKT kupata kazi za mikataba kwa shughuli mbalimbali za ulinzi wa maliasili kama wanyamapori na misitu” alisema.
Waziri huyo alikuwa akijibu swali kutoka kwa Mbunge wa Malinyi, Antipas Mgungusi aliyetaka kujua lini serikali itawatumia vijana ambao wamepata mafunzo ya JKT katika kulitumikia Jeshi la uhifadhi kwa mkataba wa muda mfupi.
Aidha, alisema Serikali imekuwa ikiwatumia vijana wa JKT walioko makambini kwa ajili ya doria za muda mfupi zinapotokea changamoto za wanyama wakali na waharibifu.