Nape: Hairuhusiwi kupandisha gharama bila mamlaka kujua

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye

WAZIRI wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye, amesema sheria za Mamlaka ya Mawasiliano nchini, haimruhusu mtoa huduma kupandisha huduma bila kupata idhini ya mamlaka husika.

Waziri Nape alikuwa akizungumzia madai ya kwamba kampuni za simu zimepandisha gharama za intaneti (bando), bila kutoa taarifa kwa watumiaji.

Hata hivyo Waziri nape alisema Ijumaa kuwa Tanzania ni miongoni mwa nchi chache Afrika na duniani, ambapo gharama za data ziko chini. Aliongeza kuwa katika kipindi cha uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, gharama za intaneti zimepungua kwa zaidi ya asilimia 76.

Advertisement

“Ukisharuhusiwa na mamlaka ni lazima utaarifu umma kabla ya kuanza kutekeleza mabadiliko hayo mapya, bahati mbaya iliyopo ni kwamba wanazituma watu hawazioni, ikipanda ndio wanasema hawakutuambia,” amesema Waziri Nape.

Waziri Nape ameitaka Mamlaka ya Mawasiliano (TCRA) na kampuni za simu kutoa majibu kwa hoja zinazoibuliwa na watumiaji wa huduma, ikiwa ni sehemu ya taasisi hizo kutoa elimu kwa Watanzania.

Amesema alitoa ofa kwamba ‘Kama kuna mtu anaamini ameibiwa aje asaidie kupata ushahidi wa huo wizi, wapo wengi wamekuja, wakishafanyiwa tathmini hawataki kuuarifu umma, na wengine ni viongozi.

Ni vizuri kuwa makini na matumizi ya simu janja,” alisema Waziri Nape.