WAZIRI wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Nape Nnauye amewataka Waandishi wa Habari kutokuwa na hofu na muswada wa sheria ya habari uliowasilishwa bungeni leo Juni 13, 2023
Nape amesema kuwa muswada huo ni rafiki licha ya baadhi ya vipengele havijaonekana katika marekebisho ya sheria, vitaingia kwenye kanuni lengo likiwa ni kuboresha sekta hivyo.
Amesema lengo la marekebisho ya muswada huo ni kuona walaji na watoaji habari wote wanapatiwa haki sawa.
“Sheria inatoa haki na wajibu kwa pande zote ikiwemo walaji na wanahabari, lakini niwatoe hofu wenzangu kuwa hiki kilikuwa kilio cha muda mrefu kwa hiyo kama kuna maeneo hayajakaa sawa watambue ziko kanuni tutaweka huko,” amesema Nape.
Marekebisho ya sheria ya Huduma ya Habari yamekuja baada ya kelele za muda wa miaka saba tangu sheria hiyo ilipotungwa mwaka 2016.
Aidha, Nape amesema kila eneo linahitaji kuwa na haki na wajibu wa marekebisho hayo yametazama pande zote kwa manufaa ya Tanzania na hasa waandishi wa habari katika kutafuta na kutoa habari zao.
Kwa mujibu wa Waziri Nape, wadau walipelekea mapendekezo katika vifungu 21 lakini kwenye mazungumzo walikubaliana vifungu nane vibaki kama vilivyo na vifungu tisa ndivyo vilivyopitiwa kwa makubaliano.