TANGA: NAIBU Waziri Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Deogratius Ndejembi amemuagiza Mkurugenzi wa Jiji la Tanga, Said Majaliwa kuwasimamisha kazi wahandisi wa Halmashauri ya Jiji la Tanga, Issa Mchezo na Mussa Mkonachi kutokana na usimamizi mbovu wa miradi huku akiagiza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) kuchunguza manunuzi katika ujenzi wa Shule ya Msingi Jaje.
Ndejembi ametoa agizo hilo jijini Tanga katika ziara yake ya kukagua miradi ya ujenzi wa Shule mpya ya Msingi Jaje iliyojengwa kupitia mradi wa BOOST na Shule ya Sekondari Magaoni iliyojengwa kwa fedha za mradi wa SEQUIP.
“TAKUKURU niwatake mlete timu yenu mara moja ya uchunguzi ili mchunguze manunuzi kwenye miradi hii. Haiwezekani Jiji la Tanga saruji iuzwe bei ya juu zaidi ya Pangani. Chunguzeni na ripoti yenu tuipate lakini pia mchukue hatua za kisheria,” amesema kiongozi huyo.
Katika ziara yake jijini humo Naibu Waziri Ndejembi pia ametembelea mradi wa soko la machinga Kange na kuzungumza na watumishi wa halmashauri ambapo amewataka kuacha kufanya kazi kwa mazoea na wawatumikie wananchi ili kutekeleza dhana ya Rais Samia ya kuhakikisha watanzania wanapata huduma iliyo bora.