DAR ES SALAAM: MSANII wa muziki wa Bongo Fleva kutoka Zanzibar, Said Seif Ally maarufu Nedy Music amesema amemchagua Barnaba katika wimbo wake mpya wa ‘Mapenzi’ kwa sababu ndiye aliyemuongoza katika kuusoma na kuufahamu muziki kwa ujumla.
Nedy Muziki anayetamba na wimbo wa ‘Nigee’ amesema hakuwahi kumshirikisha wala kuimba na mwanamuziki Barnaba tangu alipoanza muziki wake lakini katika wimbo huo amemkumbuka mtu muhimu katika maisha yake ya muziki ndiyo maana amemshirikisha katika wimbo huo.
“Nilipoandika huu wimbo wa Mapenzi niliona Barnaba anafaa licha ya ustaa wake na uwezo wa kuomba kwa kutumia vyombo lakini yeye ndiye mtu wa kwanza aliyenionyesha njia ya kuelekea muziki wangu alinipeleka Nyumba ya Vipaji (THT) nikafunzwa muziki nikawa mimi, namshukuru sana Barnabas,” amefafanua Nedy Music.
Akizungumzia maudhui ya wimbo wake huo amesema ametuma meseji kwa waliopo kwenye mahusiano ili wavumiliane waache tabia za kuachana.
“Nimeona ndoa na mahusiano mengi hayana furaha yanapitia magumu mengi badala ya furaha ndiyo maana nikatunga wimbo huu niliomshirikisha Barnabas na sasa wimbo unapatikana kote.” Amesema.