NHIF safi hospitali binafsi

Vituo 32 vyazuiwa kuhudumia wanachama wa NHIF

DAR ES SALAAM: Uongozi wa Bodi ya wamiliki wa vituo vya afya binafsi nchini (APHFTA) na Jumuiya ya Wamiliki wa Hospitali Binafsi Zanzibar (ZAPHOA), umesema umefikia uamuzi wa kurejea kwenye meza ya mazungumzo na serikali, sambamba na kurejesha huduma za afya zilizositishwa kwa wanachama wa NHIF, wakati mazungumzo hayo yakiendelea.

Taarifa ya APHFTA iliyotolewa leo, Jumamosi Machi 02, 2024 ambayo imesainiwa na Mwenyekiti wake Dk Egina Makwabe imeeleza kuwa uamuzi huo umefikiwa baada ya serikali kuonesha utayari wa kurudi katika meza ya mazungumzo kupitia mawasiliano yanayoendelea baina ya pande hizo mbili.

Wamesema uamuzi huo mgumu waliouchukua ni kielelezo cha nia na dhamira yao njema ya kutafuta suluhu ya kudumu itakayowaondolea wananchi adha ya kupata huduma za afya kwenye vituo vyao, sambamba na kuwapunguzia wamiliki gharama za utoaji wa huduma na uendeshaji.

Advertisement

APHFTA imesisitiza kuwa lengo lake ni kutoa huduma bora za afya katika mazingira ambayo yanazingatia hali ya soko na uhalisia wa gharama za uendeshaji za wamiliki wa vituo vya afya na hospitali

APHFTA imesema haina dhamira ya kuwaumiza wananchi wahitaji ambao ni wanachama wa NHIF.