DAR ES SALAAM; Mamlaka ya vitambulisho vya Taifa NIDA imewatahadharisha wananchi juu ya utapeli wa mitandaoni unaofanywa na watu wenye nia Ovu ya kujipatia fedha isivyo kihalali kutoka kwa wananchi na kuweka matangazo katika mitandao ya kijamii kuwa wanatoa Namba za utambulisho wa Taifa (NIN), Vitambulisho vya Taifa na nakala ya tape ya mtandaoni (Online Soft copy)
Taarifa ya NIDA kwa umma imebainisha kuwa baadhi ya watu wanatengeneza kurasa bandia kwenye mitandao ya kijamii na kujitangaza wanatoa huduma hizo kwa niaba ya mamlaka ya vitambulisho vya Taifa NIDA
“Tunawatahadharisha wananchi kujiepusha na watu hao kwani NIDA ndio taasisi pekee yenye mamlaka ya kisheria ya kutoa huduma hizo na wala haina wakala au mtu yoyote inayeshirikiana nae kuchapisha na kutoa namba ya vitambulisho vya NIDA pia haina huduma ya nakala tape mtandaoni (Online Soft copy)” imeeleza taarifa hiyo na kuongeza
“Tunawakumbusha wananchi kuwa malipo kwa taasisi za serikali ikiwemo NIDA hufanywa kupitia namba ya malipo ya serikali (Control number) na si kupitia namba za simu za mkononi hivyo endapo mtu yoyote atakutaka kulipia huduma yoyote ya NIDA kupitia namba za simu simu ya mkononi hayo sio malipo halali ni utapeli”
“Tunatoa Rai kwa wananchi kutumia njia na taratibu sahihi zilizowekwa na mamlaka kupitia huduma zetu za usajili na utambuzi ikiwa ni pamoja na kutumia ofisi zetu za usajili badala ya kutumia njia za mkato” imeeleza.