MWANAMITINDO Miriam Odemba amesema hajaacha kazi hiyo kama ambavyo baadhi ya mashabiki zake wamekuwa wakimnyooshea vidole kutokana na kujiingiza kwenye muziki, bali anaendelea na kazi zote kwa pamoja.
Nyota huyo aliliambia gazeti hili Dar es Salaam Alhamis kuwa anapenda muziki na mitindo hivyo, ataendelea kufanya vyote ikiwa ni sehemu ya kutafuta maisha.
Alisema anashangazwa na baadhi ya watu wakimsema vibaya tangu ameingia kuimba muziki wakisema pengine ameacha masuala ya mitindo jambo ambalo si kweli.
Na wengine wakimweleza kuwa hawezi kuimba kwa kumkatisha tamaa akisema mitandao imekuwa chanzo kikubwa cha kumpa msongo wa mawazo na hivyo kuamua kuiweka pembeni ili kuendelea na shughuli hizo nyingine.
“Kila ninapojaribu kujilinda ninaandamwa, imepitiliza. Mimi kuingia kwenye muziki mnataka niendelee na mitindo, sikuwahi kuacha, mimi ni wa kimataifa,”alisema.
Alisema kwa kuwa mitandao ya kijamii hasa Instagram imekuwa ikimpa mawazo kutokana na maneno ya watu, huenda asiingie kwa muda kwanza kujiweka sawa huku akiwaomba msamaha wote aliowakosea.
“Nawashukuru mashabiki zangu na vyombo vyote vya habari na wadau wa muziki kwa kuniunga mkono katika kipindi chote nilichokuwa nanyi,”alisema Odemba.