WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dk. Mwigulu Nchemba amesema kuwa pato la Taifa kwa mtu kwa maana kila mtanzania kwa mwaka 2022 lilikuwa Sh. Milioni 2.8 ikilinganishwa na Sh. Milioni 2.7 mwaka 2021.
Nchemba ameyasema hayo akiwasilisha taarifa ya hali ya uchumi katika mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa mwaka 2023/2024 ambapo amesema pato hilo ni sawa na ongezeko la asilimia 5.0.
Amesema, kiasi hicho cha fedha kwa mtu ni sawa na Dola za Kimarekani 1,229.1 kwa mwaka 2022 ikilinganishwa na Dola za Kimarekani 1,173.3 mwaka 2021.
Aidha, amesema hadi kufikia Aprili 2023, pato ghafi la Taifa kwa bei za mwaka husika lilikuwa Sh. Trilioni 170.3 ikilinganishwa na Sh. Trilioni 156.4 mwaka 2021.
Amesema, hadi kufikia Aprili 2023 kwa mujibu wa Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2022, idadi ya watu Tanzania Bara ilikuwa Milioni 59.8 ikilinganishwa na makadirio ya idadi ya watu Milioni 57.7 mwaka 2021.