DAR ES SALAAM: JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, limewakamata watu wanne kwa tuhuma za wizi wa magari 12 na na bajaji tano katika maeneo mbalimbali jijini Dar es salaam.
Kamanda wa Polisi kanda Hiyo, Jumanne Muliro amesema hiyo inatokana na operesheni maalum iliyoanza Desemba 2023 hadi Mei 22, mwaka huu na kwamba tayari wahusika wameshatambua magari yao.
“Watuhumiwa hao walikuwa wakiyaiba magari hayo, kufuta namba za usajili wa gari (Chesess) na kubadilisha plate namba halafu kuyauza tena yakiwa na kadi za bandia,” amesema Kamanda Muliro na kuwataja watuhumiwa hao ni Haruni Selemani (34) mkazi wa Yombo Makangarawe, Temeke na wenzake watatu.
Katika hatua nyingine Jeshi la Polisi kanda Maalum ya Dar es Salaam limemkamata Ezekiel Amani (30), mkazi wa Buza Kanisani na wenzake wawili kwa tuhuma za kuhujumu miundombinu ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO).
Watuhumiwa hao walikamatwa Mei 15, 2024 eneo la Kisarawe II, Kigamboni wakiwa wanaiba nyaya za umeme zilizokuwa juu kwenye nguzo.