Jeshi la Polisi kupitia kitengo cha kuzuia na kupambana na dawa za kulevya nchini limekamata tani 13.717 za dawa za kulevya pamoja na watuhumiwa 4987 katika maeneo mbalimbali.
Akitoa taarifa hiyo mkuu wa kitengo cha kuzuia nakupambana na dawa za kulevya nchini, kamishna msaidizi wa Polisi, ACP Amon Kakwale amesema katika kipindi cha kuanzia Januari hadi Juni 2023, kitengo hicho kilifanikiwa kukamata kiasi cha kilogramu 9,358.77 sawa na tani 9.36 za dawa za kulevya aina ya bangi.
Aidha, amesema tani 4.357 za mirungi, kilogramu 1.86 za Heroin pamoja na gramu 220.05 za Cocaine zilikamatwa na ekari 105.25 za mashamba ya bangi na mirungi yalitekeketezwa.
Katika hatua nyingine, ACP Kakwale amesema operesheni hiyo ilifanikiwa kukamata watuhumiwa 4983 ambapo kesi 3784 zilifunguliwa na zipo katika hatua mbalimbali mahakamani.
Mkuu huyo amewataka wanaonedelea kujihusisha na biashara haramu ya dawa za kulevya kuacha mara moja kwani hatua kali za kisheria zitachukuliwa kwa wote watakaojihusisha na vitendo hivyo.