Polisi yaonya wanaoshawishi wafanyabiashara

JESHI la Polisi Kanda maalum ya Dar es Salaam limesema kikundi cha watu kitakachobainika kinashawishi wafanyabiashara kutofungua biashara zao watadili nao.
Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam SACP Muliro Jumanne amesema baadhi ya wafanyabiashara wanawatisha wafanyabiashara wengine ili wafunge biashara zao.
“Wafanyabiashara wanaowatishia wengine wasifungue maduka yao tukiwabaini tutadili nao, anayetaka kufunga afunge lakini anayefungua duka asitishwe wala kufanywa chochote na Polisi tupo tunawahakikishia usalama wote waliofungua maduka yao.”Amesema na kuongeza
“Kulikuwa kuna taarifa kwamba kuna kikundi cha Watu wachache kinajaribu kuwatisha watu kwamba wasifungue maduka, tukaona kwamba sasa hapo wanavuka mipaka na kuingilia jukumu letu, suala la kutofungua au kufunga ni suala binafsi”
“Kama kuna watu wanataka kuendelea na biashara na kufungua maduka yao hawapaswi kutishwa hata kidogo, kila mtu ana uhuru wa kufanya anachotaka kufanya” Amesisitiza
“Sisi tumekuja kuona kwamba kama kuna kikundi kinapita na kuwalazimisha watu wasifanye biashara, hicho ndio kikundi ambacho itabidi tukihoji kwa kina, ndio maana ukipita baadhi ya maeneo kuna maduka yamefunguliwa na tumewahakikishia usalama”
“Natoa tahadhari juu ya kuingilia uhuru wa mtu kwenye biashara zake, anayefunga afunge lakini anayefungua asitishwe wala asifanyiwe kitu chochote, hilo ndio jukumu letu Jeshi la Polisi, tunashukuru baadhi ya Mitaa maduka yanafunguliwa”