PSSSF waipongeza serikali kulipa madeni

MFUKO wa Hifadhi ya Jamii kwa Watumishi wa Umma (PSSSF) umeipongeza serikali kwa kulipa madeni kwa mfuko huo ‘Hati Fungani’ ya Sh trilioni 2.17.

Meneja wa mfuko huo Kanda ya Mashariki inayojumuisha Mkoa wa Pwani na Morogoro, Zaida Mahava amesema hayo leo mjini Morogoro baada ya kufunguliwa mafunzo maalumu ya wastaafu watarajiwa wa PSSSF.

Alisema mafunzo hayo ya siku mbili yameshirikisha wastaafu watarajiwa 500 kutoka idara za serikali, serikali za mitaa na mashirika ya umma  katika  Mkoa wa Morogoro  na kubeba  kauli mbiu: “ Wekeza Mafao yako Sehemu Salama kwa Uhakika wa Ukwasi”.

Advertisement

Mahava alisema malipo hayo yameusaidia Mfuko wa PSSSF  kuwa na  uhakika na kufanya kazi wa kujiamini kwa sababu Mfuko una uwezo wa kulipa  mafao ya wastaafu wakiwemo wa   Kanda ya Mashariki  anayoiongoza.

“Tunaishukuru Serikali ya awamu ya sita ya  Rais Dk Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo inaunga mkono kwa  kusaidia kwa kiwango kikubwa Mfuko wetu wa  PSSSF” alisema Mahava.

Meneja wa Mfuko  wa Kanda ya Mashariki alisema moja ya sababu iliyofanywa kwa kuunganishwa kwa mifuko ilikuwa ni kutokana na baadhi ya mifuko kutokuwa na uhakika wa kulipa mafao.

Naye Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa PSSSF, Paul Kijazi alisema mwaka wa fedha wa bajeti 2023/2024 watumishi wa umma  11,000 wanatarajia kustaafu kwa mujibu wa sheria.

Kijazi ambaye ni Meneja wa Rasilimali Watu wa Mfuko huo alisema idadi hiyo inaweza kuongezeka kutokana na wale ambao wanaoomba kustaafu utumishi wa umma  kwa hiari wanapofikisha umri wa miaka 55.

Pamoja na hayo  alisema kuwa Mfuko wa  PSSSF  kwa sasa inawahudumia  wastaafu waliopo kwenye mfumo wa malipo ya kila mwezi  wapatao 160,000.

Katika hatua nyingine Mfuko wa PSSSF umeanzisha mpango mkakati wa kuunga mkono serikali katika suala la kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi  na kuweka lengo la mwaka huu  kupanda miti milioni tano.

Kwenye  mafunzo ya  wastaafu watarajiwa  hao walipatiwa  miti ya matunda,  kila mmoja alipewa miche miwili kwa ajili ya kwenda kuotesha baada ya kupatiwa elimu  wataalamu wa kilimo kuhusu namna uoteshaji na utunzaji.

Add a comment

Toa Jibu

Barua-pepe haitachapishwa. Fildi za lazima zimetiwa alama ya *