Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) imekutana na kufanya mazungumzo na Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Hanafi Msabaha kuelezea umuhimu wa kuwa na Mwongozo wa uwajibikaji wa kampuni kwa jamii (CSR).
Katika kikao hicho, rasimu ya mwongozo uliondaliwa na PURA umewasilishwa.
Imeelezwa kuwa mwongozo huo utasaidia utekelezaji wa miradi ya CSR inayotekelezwa na kampuni za utafutaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia nchini.
Mazungumzo hayo yamefanyika Julai 20, 2023 katika Ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Mtwara na kuhudhuriwa na wajumbe mbalimbali akiwemo Katibu Tawala Wilaya ya Mtwara, Wakurugenzi wa Hamlashauri za Manispaa za Mtwara mjini na vijijini na wataalamu kutoka PURA na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mtwara.A
kizungumza wakati wa kuwasilisha rasimu hiyo, Mkurugenzi Mkuu wa PURA Charles Sangweni alisema kuwa chimbuko la kuandaliwa kwa Mwongozo wa uwajibikaji wa kampuni kwa jamii ni Kifungu Namba 222(4) cha Sheria ya Petroli ya Mwaka 2015 na kwamba ni wakati muafaka sasa kuweka mwongozo utakaowezesha utekelezaji wa miradi ya CSR inayozingatia mahitaji na vipaumbele vya jamii.
“Sisi kama PURA wakati mwingine tunapozunguka kukagua utekelezaji wa miradi ya CSR na kuhoji uongozi wa jamii husika kama ulishirikishwa katika kupanga aina ya mradi wa kutekeleza, tunakuta kwamba baadhi ya miradi haikuzingatia vipaumbele vya jamii husika, hali inayopelekea mradi kutelekezwa au kutokutumiwa kulingana na matarajio” alisema Sangweni.
Akichangia mara baada ya wasilisho la PURA, Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Mhe.Hanafi alieleza kuwa Mwongozo huo ni muhimu na kuipongeza PURA kwa kuchagiza uaandaaji wa Mwongozo huo.
“Ombi langu kuu ni kwamba Muongozo huu ujumuishe namna ya kukokotoa kiasi ambacho kampuni zitatakiwa kuchangia katika miradi ya CSR kwani kwa sasa hakuna fomula maalum ya kukokotoa kila kampuni ichangie vipi kulingana na faida inayotengeneza au ukubwa wa uwekezaji” aliongeza Mhe. Hanafi.
Pamoja na pendekezo la kuwa na kanuni maalum, Hanafi aliomba pia, kama itawezekana, kuwepo kwa mwongozo mmoja kwa sekta zote kwani CSR sio kwenye sekta ya mafuta na gesi asilia pekee.