DODOMA: WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mohamed Mchengerwa amewasilisha ripoti ya kumkumbusha Rais Samia Suluhu Hassan kuhusu mikopo ya halmashauri ili mchakato wa utoaji wa mikopo hiyo urejee.
Rais Samia Suluhu Hassan alisitisha mikopo hiyo ya halmashauri baada ya kupokea ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali na kuelekeza yafanyike mapitio ya namna mikopo hiyo itakavyotolewa.
Naibu Waziri Ofisi ya Rais TAMISEMI Deogratius Ndejembi ameyasema hayo Bungeni Dodoma alipokuwa akijibu swali la Mbunge Mwantumu Zodo aliyetaka kufahamu ni lini Serikali itarejesha mikopo ya asilimia 10 ya halmashauri ambayo imesitishwa kwa muda mrefu, na kama bado kwa nini halmashauri zinaendelea kutenga fedha hizo kila robo ya mwaka.
Akijibu swali hilo Ndejembi amesema “na hivi tunavyozungumza Mheshimiwa Spika Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI (Mohamed Mchengerwa) amekumbushia kwa Mheshimiwa Rais hili jambo ili liweze kurudi sasa na kuanza utekelezaji wake , kama kuna sheria ya kubadilika iletwe mbele ya Bunge hapa ili sheria hizo ziweze kubadilika”.
Ameongeza kuwa kwa mujibu wa sheria ya fedha ya Serikali za mitaa, halmashauri zinaendelea kutenga fedha hizo za mikopo na endapo mikopo hiyo itatakiwa kutolewa fedha zipo.