Rais Samia ameleta mapinduzi kwenye sekta ya utalii

MOROGORO: KAMATI ya Kudumu ya Bunge , Ardhi , Maliasili na Utalii imeridhishwa na utekelezaji wa  kazi za miradi ya Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya  Covid -19 iliotekelezwa na Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania  ( TAWA).

Mamlaka hiyo  kupitia mpango huo iliidhinishiwa Sh bilioni 12.9  kati ya fedha hizo Sh bilioni 9.2 ni kwa ujenzi wa miundombinu kwenye miradi 32 , Sh bilioni 3.7 ununuzi wa magari sita , mitambo mitatu na boti za kisasa sita.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo Timotheo Mnzava  alitoa pongezi kwa Mamlaka hiyo   baada ya  kutembelea na kufanya ukaguzi wa miradi  uliyokamilika eneo la Pori la Akiba Wami- Mbiki ambalo  kwenye  Mkoa wa Pwani kwa asilimia kubwa pamoja na Morogoro.

Advertisement

Hivyo alimpongeza Rais , Dk Samia Suluhu Hassan kwa ubunifu wake wa kutafuta  fedha na maelekezo aliyoyatoa juu ya matumizi ya fedha hizo za Covid -19 ambazo zimeleta mapinduzi makubwa katika sekta  utalii na nyinginezo .

“ Tunampongeza kwa ubunifu mkubwa alionao kwa kutafuta fedha kwa sababu miradi mingi imetekelezwa kwa kutumia fedha Covid-19 na ndiye aliyezitafuta na kuzitolea maelekezo namna gani zitumike” alisema  Mnzava.

“ Kwa mazingira na hali tuliyoiona kwenye Pori hili la Wami – Mbiki  nadhani tutaungana sote kumpongeza kwa dhati Rais wetu Dk Samia  kwa kazi nzuri anayoifanya kwenye nchi yetu” alisisitiza  Mnzava .

Mwenyekiti wa kamati huyo  alitoa  wito na ushauri kwa wizara kuongeza mikakati ya kibiashara na ya kimasoko kutangaza mapori hayo ili miundombinu iliyotengenezwa itumike ilivyokusudiwa kwa ajili ya kupata  tija iliyotarajiwa.

Naye  Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Dunstan  Kitandula alisema wizara imejipanga  kuhakikisha inaongeza jitihada katika kutangaza hifadhi hiyo ili kuongeza idadi ya  wageni ikiwa ni pamoja na kutafuta wabia wa kushirikiana nao katika kuendesha  shughuli za utalii na uwekezaji.

Kitandula alisema  Mamlaka hiyo ilikabidhiwa pori hilo kwa ajili ya kuliboresha , kulirejesha katika hali yake ya uoto wa asili na kuhakikisha idadi ya wanyamapori kwa kwenye pori hilo inaongezeka.

Kwa upande wake Kamishna  wa Uhifadhi wa Mamlaka hiyo , Mabula Misungwi Nyanda aliithibitishia Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi , Maliasili na Utalii , kuwa miradi yote iliyokuwa inatekelezwa kwa kiasi hicho cha fedha imekamilika.

TAWA  iliidhinishiwa kiasi cha Sh bilioni 12.9  na  kati ya fedha hizo Sh bilioni 9.2 ni kwa ujenzi wa miundombinu  kwenye miradi 32 , wakati  Sh bilioni 3.7 ni ununuzi wa magari sita , mitambo mitatu na boti za kisasa sita.

Nyanda alisema ,kwa hivi sasa wameendelea kuzishikilia fedha za Covid-19 Sh milioni 19.8 ambazo ni za   matazamio ya mradi (Retention)   ya ujenzi wa  daraja la Pori la Akiba Mpanga  Kipengere ambalo kipindi cha  matazamio ( Defects Liability Period ) kitakamilika  Agosti 2024.

“ Ninakuhakikishia Mwenyekiti wa Kamati sisi miradi yote iliyokuwa inatekelezwa chini ya fedha za Covid-19 tumeikamilisha  “ alisema Kamishna Nyanda.