RAIS Samia Suluhu Hassan amewataka viongozi wa serikali ikiwemo mawaziri, manaibu Waziri kuacha kuajiri maafisa habari binafsi, badala yake watumie vitengo vya habari kutoa taarifa za serikali.
Rais Samia ameyasema hayo leo, Machi 2, 2023 akifungua mkutano wa faragha wa Mawaziri, Manaibu Waziri, Makatibu Wakuu na Naibu Makatibu Wakuu katika Ukumbi wa Mikutano wa Arusha (AICC).
Amesema, Mawaziri wengi wameajiri maafisa habari wao binafsi ambao wanatoa taarifa zao na kuacha kutoa taarifa za serikali.
Muwe wepesi kutoa taarifa, kila wizara ina vitengo vya Habari vinatumikaje, vimekaa tu, mawaziri mmeajiri maafisa habari wa kutoa taarifa zenu sio za wizara, twendeni mkarekebishe.”Amesema Rais Samia
Aidha, amewataka viongozi hao kutengeneza utaratibu wa kupashana habari, kufanya kazi kwa weledi, kuwa na mawasiliano ya karibu ili kuondoa kauli tatanishi ambazo zinaleta mgongano katika jamii.
“Unakuta Wizara moja, uyu anasema hili, kesho yule anasema lile, hakuna mawasiliano, kauli zimekua zinatolewa tofauti na kuleta mkanganyiko.”Amesema
Rais Samia pia amewataka Mawaziri kuwa wepesi kuisemea serikali pale wanasiasa wanapofanya upotoshaji.
“Katika eneo la kuisemea serikali hatujafanya vizuri, tumekuwa wazito kufanya hivyo na kuacha watu wengine wakifanya upotoshaji…..Kuna msemo uongo ukisemwa mara nyingi uwa kweli, serikali yetu imefanaya mambo mengi ya kutatua shida za wananchi lakini hayasemwi.
Amesema, kuna kauli nyingi za upotoshaji zimekuwa zikitolewa na wanasiasa kuhusu utendaji wa serikali akitolea mfano mmoja wa kiongozi ambaye alitoa kauli ya kuilaumu serikali kutumia pesa nyingi kutafuta vyanzo vya maji, wakati kuna visima vingi vilichimbwa miaka ya nyuma.
“Nimewahi kuona kiongozi wa kisiasa akiilaumu Serikali inatumia fedha nyingi kutafuta vyanzo vipya vya maji kupeleka kwa wananchi, ilhali kuna visima kadhaa vilichimbwa nyuma na serikali iliviacha.
“Wizara inayohusika na hili, ilipaswa kusimama haraka kujibu kwa kutoa facts (ukweli), fugures (takwimu) na kumueleza kwanini visima hivyo viliachwa na kwamba vimeachwa au havikuachwa, mambo kama haya muwe wepesi kutoa majawabu mtu anapopotosha.