RAIS Samia Suluhu Hassan amewataka mablozi wateule kujifunza zaidi jinsi mataifa mengine yanavyofanya katika ukuaji wa uchumi wa mataifa yao, ili wahamishie ujuzi huo nchini, kwani kazi yao sio kufanya uwakilishi tu wa Tanzania katika mataifa hao.
Akizungumza mara baada ya uapisho wa mabalozi hao aliowateua, Rais Samia amesema wapo mabalozi ambao wanaonekana pale ambapo ujumbe wa Tanzania umekwenda kwenye nchi hiyo, anapokea wageni, anawasindikiza , au Watanzania wafanye ukorofi ndio utaona ripoti ya balozi, au unamuona siku za sherehe za kitaifa za nchi hiyo, lakini mengine hakuna, hakuna la maana linalotoka huko.
“Katika nchi nyingine mabalozi wetu sijui niseme hawajui wanachokifanya, wapo tu. Nilikutana na Rais mwenzangu ndani ya SADC akaniambia nimbadilishie balozi kwa kuwa aliyepo kazini haendi na mikutano hashiriki.
“Sasa nyinyi nataka mkafanye kazi, mtuambie wenzetu wamefanya uchawi gani kukua kiuchumi na sisi tunakosa nini, tuna rasilimali hatuzitumii? Au kitu gani, ila niseme wazi wenzetu wamepiga hatua kubwa sana licha ya kuwa sisi tumewazidi kwenye rasilimali, diplomasia ya uchumi ifanye kazi hapa, tujiulize tuliachwa wapi?”Amehoji.
Rais Samia ameiagiza Wizara ya Mambo ya Nje kuweka mfumo utakaoonesha kazi zote zinazofanywa na balozi za Tanzania katika mataifa mbalimbali, huku akihimiza matumizi ya TEHAMA katika kurahisisha na kuharakisha kazi.
Mabalozi walioapishwa leo na nchi wanazokwenda kwenye mabano ni Fatma Mohamed Rajabu kuwa Balozi wa Tanzania nchini Omani, Joseph Sokoine (Canada), Naimi Hamza Azizi (Austria).
Meja Jenerali Ramson Mwaisaka (Rwanda), Meja Richard Makanzo (Cairo Misri), Gelasius Byakanwa (Burundi), Habibu Awesi Mohamed (Qatar) na Mahadhi Juma Maalim (Kuala Lumpur, Malaysia).
Pia wapo Imani Njalikai (Algeria), Hassan Idd Mwamweta (Ujeruamani), Abdallah Saleh Posi (Geneva, Uswisi) Dk Mohamed Juma Abdallah (Saudi Arabia) na Jabir Mwadini (Ufaransa).