MKUU wa Mkoa wa Mtwara Kanali Ahmed Abbas amewaonya baadhi ya wafanyabiashara wanaohujumu zoezi la usafirishaji wa korosho kupitia Bandari ya Mtwara katika msimu wa 2023/24.
Akizungumza Novemba 8, 2023 alipofanya ziara ya kushtukiza bandarini hapo ili kujionea namna ambavyo zoezi hilo linaendelea, Mkuu huyo wa mkoa amesema kuwa kuna viashiria vya hujuma zinazofanywa na watu wenye nia mbaya ya kutaka kukwamisha jitihada za serikali za kukuza pato la mkoa kupitia zao hilo.
Akiwa bandarini hapo RC Abbas ameshuhudia foleni ya malori yaliyokuwa yakisubiri kuingia ndani kupakua korosho hivyo kulamzimika kutoa maagizo kwa wasimamizi wa kampuni mbalimbali za usafirishaji zinazohusika na zoezi hilo la usafirishaji wa bidhaa hiyo.
‘’Ndugu zangu nimeingia ndani na kutembelea kila eneo hakuna shida nimekagua makasha nimejionea yapo ya kutosha yanasubiri mzigo uingie upakuliwe ninachotaka kufahamu…… kwa nini ndani hakuna lori linaloshusha mzigo lakini hapa nje kuna foleni ya aina hii!!!’’amesema Abbas.
Hata hivyo amewataka wadau wa usafirishaji hao waliyokuwa wakisubiri kuteremsha mizigo yao bandanini hapo kuwa, tayari serikali imebaini kuwa baadhi ya wafanyabiashara wamekuwa wakila njama ya kuhujumu zoezi hilo kwani serikali ya mkoa itachukuwa hatua kwa yeyote atakayebainika kuhusika na vitendo hivyo.
Aidha ametoa maagizo kwa wasafirishaji hao kuwa magari yote yaliyopo nje kwenye foleni bandarini hapo yaingie ndani mara moja yaanze kushusha mzigo na kama kuna mtu anataka kusafirisha korosho kwa njia ya barabara apeleke maombi wata yatathimini na kama yatakuwa na mashiko wataruhusu.
‘’Hatutaruhusu figisu figisu katika suala kama hili lenye maslahi makubwa kwa taifa letu, kuanzia sasa naagiza magari yote yaliyopo hapa nje kwenye foleni yaingie ndani mara moja yaanze kushusha mzigo’’amesema Abbas
Zoezi hilo la kusafirisha korosho zote zinazozalishwa katika mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma kupitia bandari hiyo ni utekelezaji wa agizo la Rais Samia Suluhu Hassan wakati wa ziara yake aliyoifanya hivi karibuni mkoani humo.
Lengo likiwa ni pamoja na kuhakikisha kuwa kila Mwananchi ananufaika na mnyororo wa thamani katika zao hilo.
Aidha mpaka kufikia Novemba 7, 2023 jumla ya makasha 335 sawa na tani 8,275 elfu zilikuwa tayari zimeandaliwa bandarini hapo zikisuribi kusafirishwa kwenda katika nchi mbalimbali duniani.