KOCHA Mkuu wa Simba, Roberto Oliveira ‘Robertinho’ amesema ushindi wa mabao 5-1 walioupata jana dhidi ya Ihefu FC, ni maandalizi ya michezo yao miwili mikubwa dhidi ya Yanga na ule wa robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Wydad Casablanca.
Akizungumza na HabariLEO, kocha amesema pamoja na ushindi huo mnono lakini akili zao wamezielekeza kwenye mechi hizo mbili sababu nimechi kubwa na malengo yao ni kuhakikisha wanashinda.
“Mchezo dhidi ya Ihefu ulikuwa muhimu pia lakini kipaumbele chetu cha kwanza kwa sasa ni kushinda mechi ya Derby dhidi ya Yanga na mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Wydad Casablance na hilo linawezekana sababu kila siku timu yangu imekuwa ikiimarika kiuchezaji,” amesema Robertinho.
Simba itacheza na Yanga Aprili 16 huo ukiwa ni mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara siku chache baadae Aprili 23 itawakabili mabingwa wa Afrika Wydad Casablanca mchezo utakaopigwa katika dimba la Benjamin Mkapa, Dar es Salaam.