Samia ataka uwekezaji wa sayansi, teknolojia

RAIS Samia Suluhu Hassan, amesema Tanzania na Afrika wakiwekeza zaidi katika sayansi na teknolojia kwa vijana, wanaweza kuwa sehemu muhimu ya kustawisha uchumi kama ilivyo China.
Ametoa kauli hiyo Dar es Salaam leo, wakati akifungua Mkutano wa Wanawake na Vijana katika Biashara chini ya Mkataba wa Eneo Huru la Biashara la Afrika, ambao unawakutanisha viongozi na wadau mbalimbali kutoka Afrika.
Amesema ni muhimu wanawake na vijana wakajengewa uwezo kupitia elimu, ikiwa ni pamoja na kutumia sayansi na teknolojia itakayowawezesha kumiliki na kutumia rasilimali za Afrika, kujenga na kukuza Afrika ya viwanda na biashara kwa uchumi imara.
“Tutakapokwenda kutekeleza hili, tutaangalia lengo namba mbili ambalo linaangazia biashara Afrika, ambalo linasisitiza kuhusu kuwa na raia walioelimika, wenye maarifa ambao wanaweza kwenda sambamba na kasi ya sayansi na teknolojia,”amesema.
Rais Samia amesema kuwa: “Ninataka kutilia mkazo suala la elimu kwa vijana kuhusu sayansi na tekolojia, na mfano mzuri ni kwa nchi ya China, ambayo uchumi wake kupitia sayansi na teknolojia unajengwa na vijana wenye umri wa miaka 18 hadi 35, unaweza kukuta maprofesa wengi wa miaka 35, ambao wamebobea katika masuala ya sayansi na teknolojia na ndiyo wanaongoza makampuni mengi yanayozalisha sana kwenye nchi yao.