SERIKALI imekata rufaa dhidi ya hukumu iliyotolewa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha juu ya kesi ya Uhujumu uchumi iliyokuwa ikimkabili aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai mkoani Kilimanjaro Lengai Ole Sabaya na wenzake watano.
Sebaya na wenzake watano waliachiwa huru Juni 10 mwaka huu baada ya Hakimu, Patricia Kisinda wa Mahakama hiyo kubaini ushahidi uliotolewa na Jamhuri uligubikwa na utata na hivyo kushindwa kuthibitisha mashtaka.
Mbali na Sabaya wajibu rufaa wengine ni Enock Mnkeni, John Aweyo, Sylvester Nyegu, Jackson Macha na Nathan Msuya.
Sabaya alikuwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi akikabiliwa na mashtaka mengine, hata hivyo aliomba Mahakama hiyo kuiahirisha kesi yake kwa kuwa hakuwa na mawakili Mahakamani hapo. Vile vile amefikishwa katika Mahakama Kuu kanda ya Arusha ambayo imepanga kusikiliza rufaa hiyo.
Taarifa iliyotolewa Mahakamani hapo, rufaa hiyo itaanza kusikilizwa kesho, Disemba 13.