Serikali yasajili NGOs mpya 1,418

DODOMA: Serikali imesajili Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGOs) 1,418 kwa mwaka 2023, ikilinganishwa na Mashirika 1,351 yaliyosajiliwa mwaka 2022, sawa na ongezeko la asilimia 9.8.
Kwa mujibu wa Taarifa ya Wizara ya Fedha ni kuwa ongezeko hilo lilitokana na matumizi ya mfumo wa kielektroniki katika usajili wa Mashirika.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa kati ya mashirika yaliyosajiliwa, Mashirika 63 yalikuwa ya Kimataifa, 1,357 ngazi ya Taifa, 38 ngazi ya mkoa na 26 ngazi ya wilaya. 419.
Aidha mwaka 2023, utendaji kazi wa mashirika 2,824 Yasiyo ya Kiserikali ulifuatiliwa ikilinganishwa na mashirika 1,605 mwaka 2022.
Kati ya hayo, Mashirika 397 yalitembelewa na Mashirika 2,427 yalifikiwa kupitia mkutano. Ufuatiliaji huo ulibaini kuwa, Mashirika mengi yalitekeleza miradi yenye tija kwa jamii ikiwemo: ujenzi wa vyumba vya madarasa na matundu ya vyoo kwa shule za msingi na sekondari.
SOMA: Serikali: Umeme umefika vijiji 11,973
Pia ujenzi wa vituo vya afya; elimu kuhusu haki ya wanawake kumiliki ardhi na rasilimali; kuongeza thamani katika mazao ya kilimo; uwezeshaji wananchi kiuchumi; elimu ya afya, ulinzi na usalama wa mtoto; na utoaji wa bima ya afya ya jamii. Aidha, mikataba 500 ya fedha ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ilikaguliwa mwaka 2023 ikilinganishwa na mikataba 955 mwaka 2022.
Vile vile, ukaguzi wa mikataba ya fedha ulibaini kuwa Sh bilioni 671.44 zilipokelewa mwaka 2023 ikilinganishwa na Sh bilioni 1,081.50 mwaka 2022.