DODOMA; SERIKALI imetaka waajiri wote nchini kuhakiki na kuwasilisha madeni ya watumishi kwa ajili ya taratibu za uhakiki na malipo.
Kauli hiyo imetolewa bungeni leo na Naibu Waziri Ofisi ya Rais (Utumishi na Utawala Bora), Ridhiwani Kikwete alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum, William Mgaya aliyehoji ni lini serikali itamaliza kulipa madeni ya muda mrefu ya watumishi.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri Kikwete amesema, serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kudhibiti uzalishaji wa madeni ya watumishi ikiwemo malimbikizo ya mishahara kwa kujenga Mfumo Mpya wa Taarifa za Kiutumishi na Mishahara (HCMIS), ulioanza kutumika mwezi Mei, 2021, ambao umeweza kudhibiti uzalishaji wa malimbikizo mapya ya Mishahara.
“Pamoja na hatua hiyo, kuanzia mwezi Mei, 2021 hadi sasa Serikali imelipa madai ya malimbikizo ya mishahara ya watumishi 132,611 yenye thamani ya Shilingi 219,732,820,025.74.
“Aidha, Serikali inatoa wito kwa waajiri wote nchini kuhakiki na kuwasilisha madeni ya watumishi kwa ajili ya taratibu za uhakiki na malipo,” amesema Naibu Waziri huyo.