Sh Bil 2 kupelekwa Barabara Inyala

WAZIRI wa Ujenzi na Uchukuzi, Prof. Makame Mbarawa, amemuagiza Katibu Mkuu wa Ujenzi, Balozi Aisha Amour, kupeleka kiasi cha Sh bilioni mbili katika ofisi ya Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Mbeya, ili kusaidia kuboresha barabara eneo la Inyala, ambapo kumekuwa na mfululizo wa ajali za mara kwa mara.
Ametoa agizo hilo mkoani Mbeya, mara baada ya kukagua eneo la Mlima Nyoka hadi mteremko wa Shamwengo, ambapo pamoja na mambo mengine Prof. Mbarawa amesisitiza kuwa fedha hizo zifike haraka, kwani mkandarasi ameshapatikana na kuanza kazi za awali za maboresho ya eneo hilo zinaendelea, ili kukamilisha ujenzi wa barabara ya mchepuko km 2.8 kwa kiwango cha lami, pamoja na uwekaji wa taa za barabarani.
“Eneo hili limekuwa na changamoto za ajali za mara kwa mara hivyo, nimeamua kuja kukagua hapa, ili kushuhuhudia kazi zinazoendelea kufanyika, ni imani yangu kuwa kukamilika kwa kazi hii kutapunguza changamoto za ajali na magari yataendelea kupita bila kupata changamoto zozote”, amesema Prof. Mbarawa.
Prof. Mbarawa amebainisha mipango ya muda mfupi iliyochukuliwa ili kupunguza ajali katika eneo hilo, ni pamoja na kujenga sehemu za kuegesha magari, ili kuwapa nafasi polisi kufanya ukaguzi wa magari ya masafa marefu, kabla ya kuyaruhusu kuendelea na safari, pindi wanapokaribia kupita eneo la Inyala na kuongeza idadi ya alama za tahadhari kuimarisha usalama wa eneo hilo.