SERIKALI imetoa Shilingi Bilioni 8 kwa ajili ya kutekeleza miradi ya Maji, wilayani Mtwara.
–
Miradi hiyo inatekelezwa na Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Vijijiini (RUWASA), ikiwemo miradi mipya pamoja na ile inayoendelea wilayani humo.-
Hayo yameelezwa leo katika Mkutano Mkuu wa nusu mwaka wa wadau wa maji Wilaya ya Mtwara mwaka 2020/22, uliofanyika Manispaa ya Mtwara Mikindani, mkoani Mtwara.
–
Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Dunstan Kyobya, ameielekeza mamlaka hiyo kuongeza ufanisi na kasi ya utendaji wake wa kazi katika utekelezaji wa miradi hiyo, kuongeza kasi ya ununuzi ili utekelezaji huo uweze kwenda na wakati, ili wananchi wa maeneo hayo waweze kupata huduma hiyo.
–
“Ruwasa hakikisheni kwamba utaratibu wa manunuzi unaongeza kasi hatuwezi kuwa na fedha miezi sita, halafu kazi haifanyiki,” amesema Kyobya.
Meneja wa Ruwasa Wilaya ya Mtwara, Mhandisi Hamisi Mashindika, amesema kwa sasa huduma ya maji wilayani humo ipo kwa asilimia 59 na hadi kukamilika kwa miradi hiyo ambayo inatekelezwa wilayani humo itawaongezea asilimia 20, ambayo itawahudumia watu 76,000.
Mbunge wa Jimbo la Nanyamba, Abdallah Chikota ameipongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuanzisha Bodi ya Manunuzi ya Kanda ya Kusini, ambayo awali haikuwepo inayoshughulikia suala la Manunuzi kwa Mikoa ya Mtwara na Lindi, itakayosaidia kutekeleza miradi hiyo kwa wakati.